Deuteronomy 12

Mahali Pekee Pa Kuabudia

1 aHizi ndizo amri na sheria ambazo ni lazima mwe waangalifu kuzifuata katika nchi ambayo Bwana, Mungu wa baba zenu, amewapa kumiliki, kwa muda wote mtakaoishi katika nchi. 2 bHaribuni kabisa kila mahali pao pa kuabudia kwenye milima mirefu, vilima na chini ya kila mti mkubwa ambamo mataifa haya mnayokwenda kuchukua ardhi yao huabudia miungu yao. 3 cBomoeni madhabahu zao, vunjeni yale mawe wanayoabudu, chomeni moto nguzo zao za Ashera; katilieni mbali sanamu za miungu yao na mfute majina yao mahali hapo.

4 dKamwe msimwabudu Bwana Mwenyezi Mungu wenu kama wanavyoabudu wao. 5 eBali mtatafuta mahali Bwana Mwenyezi Mungu wenu atakapopachagua katika makabila yenu yote ili aliweke jina lake huko kuwa makao yake. Mahali hapo ndipo iwapasapo kwenda; 6 fhapo ndipo mtakapoleta sadaka zenu za kuteketezwa na dhabihu, zaka zenu na changizo zenu, kile ulichoweka nadhiri kutoa, sadaka zenu za hiari na malimbuko ya makundi yenu ya ng’ombe pamoja na mbuzi na kondoo. 7 gHapo, katika uwepo wa Bwana Mwenyezi Mungu wenu, ninyi pamoja na jamaa zenu, mtakula na kufurahia kila kitu ambacho mmegusa kwa mikono yenu, kwa sababu Bwana Mwenyezi Mungu wenu amewabariki.

8 hMsifanye kama tunavyofanya hapa leo, kila mtu anavyopenda mwenyewe, 9 ikwa kuwa bado hamjafikia mahali pa mapumziko na urithi ambao Bwana Mwenyezi Mungu wenu anawapa. 10 jLakini mtavuka Yordani na kuishi katika nchi Bwana Mwenyezi Mungu wenu anayowapa kama urithi, naye atawapa pumziko kutokana na adui zenu wote wanaowazunguka ili ninyi mpate kuishi kwa salama. 11 kKisha kuhusu mahali Bwana Mwenyezi Mungu wenu atakapopachagua kuwa mahali pa makao ya Jina lake, hapo ndipo inapowapasa kuleta kila kitu ninachowaamuru: sadaka zenu za kuteketezwa na dhabihu, zaka zenu na changizo, pamoja na vitu vyote vyenye thamani ambavyo mmeweka nadhiri kumtolea Bwana. 12 lHapo furahini mbele za Bwana Mwenyezi Mungu wenu, ninyi, wana wenu na binti zenu, watumishi wenu wa kiume na wa kike, pamoja na Walawi kutoka miji yenu ambao hawana mgawo wala urithi wao wenyewe. 13 mKuweni waangalifu, msitoe dhabihu zenu za kuteketezwa mahali popote mnapopapenda. 14Mtazitoa tu mahali pale ambapo Bwana atachagua katika mojawapo ya makabila yenu, nanyi hapo zingatieni kila jambo ninalowaamuru.

15 nHata hivyo, mnaweza kuwachinja wanyama wenu katika miji yenu yoyote ile na kula nyama nyingi mpendavyo kama vile mmemchinja paa au kulungu, kulingana na baraka mtakazojaliwa na Bwana Mwenyezi Mungu wenu. Watu walio najisi au walio safi wanaweza kula. 16 oLakini kamwe usinywe damu; imwage juu ya ardhi kama maji. 17 pHamruhusiwi kula katika miji yenu zaka yenu ya nafaka, ya divai mpya na ya mafuta, au mzaliwa wa kwanza wa makundi yenu ya ng’ombe na makundi yenu ya mbuzi na kondoo, wala chochote ambacho mmeweka nadhiri kukitoa, au sadaka zako za hiari, wala matoleo maalum. 18 qBadala yake, mtakula vitu hivyo katika uwepo wa Bwana Mwenyezi Mungu wenu mahali ambapo Bwana Mwenyezi Mungu wenu atapachagua: wewe, wana wako na binti zako, watumishi wako wa kiume na wa kike, na Walawi kutoka miji yenu. Mnatakiwa mfurahi mbele za Bwana Mwenyezi Mungu wenu kwa kula kitu mtakachoweka mikono yenu. 19 rMwe waangalifu msiwapuuze Walawi kwa muda wote mnaoishi katika nchi yenu.

20 s Bwana Mwenyezi Mungu wenu atakapokuwa ameongeza nchi yenu kama alivyowaahidi, nanyi mkitamani nyama na mkisema, “Ningependa nyama,” hapo unaweza kula nyingi upendavyo. 21 tKama mahali ambapo Bwana Mwenyezi Mungu wenu atapachagua kuweka Jina lake ni mbali sana kutoka kwenu, unaweza kuchinja wanyama kutoka makundi yenu ya ng’ombe, ya mbuzi na ya kondoo ambayo Bwana amewapa, kama nilivyokuamuru, na mkiwa katika miji yenu wenyewe mnaweza kula nyingi mtakavyo. 22Mle kama vile mngekula paa na kulungu. Wote walio najisi kiibada na walio safi mwaweza kula. 23 uLakini hakikisheni kwamba hamkunywa damu, kwa sababu damu ni uhai, kamwe msile uhai pamoja na nyama. 24Hamruhusiwi kamwe kunywa damu; imwageni juu ya ardhi kama maji. 25 vMsinywe damu, ili mweze kufanikiwa ninyi pamoja na watoto wenu baada yenu, kwa sababu mtakuwa mkifanya lililo haki machoni pa Bwana.

26 wLakini vichukueni vitu vyenu vilivyowekwa wakfu pamoja na vile mlivyoweka nadhiri, mwende mahali pale Bwana atakapopachagua. 27 xLeteni sadaka zenu za kuteketezwa juu ya madhabahu ya Bwana Mwenyezi Mungu wenu, vyote nyama na damu. Damu ya dhabihu zenu lazima imiminwe kando ya madhabahu ya Bwana Mwenyezi Mungu wenu, lakini nyama mnaweza kula. 28 yMwe waangalifu kutii masharti haya yote ninayowapa, ili kwamba siku zote mweze kufanikiwa, ninyi pamoja na watoto wenu baada yenu, kwa sababu mtakuwa mkifanya lililo jema na sahihi mbele za macho ya Bwana Mwenyezi Mungu wenu.

29 z Bwana Mwenyezi Mungu wenu atayakatilia mbali mbele yenu mataifa ambayo punde kidogo mtayavamia na kuyaondoa. Lakini mtakapokuwa mmeyafukuza na kuishi katika nchi yao, 30 aana baada ya kuangamizwa mbele yenu, mwe waangalifu msijiingize katika tanzi kwa kuuliza habari za miungu yao, mkisema, “Je, mataifa haya hutumikiaje miungu yao? Nasi tutafanya vivyo hivyo.” 31 abKamwe msimwabudu Bwana Mwenyezi Mungu wenu kwa njia wanayoabudu miungu yao, kwa sababu katika kuabudu miungu yao, wanafanya aina zote za machukizo anayoyachukia Bwana. Hata huwateketeza wana wao na binti zao kwa moto kama kafara kwa miungu yao.

32 acAngalieni kwamba mnafanya yote niliyowaamuru; msiongeze kitu wala msipunguze kitu.
Copyright information for SwhKC